Deuteronomy 20

Kwenda Vitani

1 aMtakapokwenda vitani kupigana na adui zenu na mkaona farasi na magari ya vita na jeshi kubwa kuliko lenu, msiwaogope, kwa sababu Bwana Mwenyezi Mungu wenu aliyewatoa kutoka Misri, atakuwa pamoja nanyi. 2Wakati mtakapokaribia kwenda vitani, kuhani atakuja mbele na kuhutubia jeshi. 3 bAtasema: “Sikia, ee Israeli, leo unakwenda vitani kupigana na adui zako. Usife moyo wala usiogope, usitishwe wala usitiwe hofu mbele yao. 4 cKwa kuwa Bwana Mwenyezi Mungu wenu ndiye huenda pamoja nanyi kuwapigania dhidi ya adui zenu na kuwapatia ushindi.”

5 dMaafisa wataliambia jeshi: “Je, kuna yeyote aliyejenga nyumba mpya ambayo haijawekwa wakfu? Yeye na arudi nyumbani, ama sivyo anaweza kufa vitani na mtu mwingine akaiweka wakfu. 6 eJe, kuna yeyote aliyepanda shamba la mizabibu na hajaanza kulifurahia? Yeye na arudi nyumbani, au sivyo anaweza kufa vitani na mtu mwingine akalifurahia. 7 fJe, kuna yeyote aliyeposa mwanamke na hajamwoa? Yeye na arudi nyumbani, ama sivyo anaweza kufa vitani na mtu mwingine akamwoa.” 8 gKisha maafisa wataongeza haya, “Je, kuna mtu anayeogopa ama kufa moyo? Yeye na arudi nyumbani ili ndugu zake nao wasije wakafa moyo pia.” 9Wakati maafisa watakapomaliza kuzungumza na jeshi, watawateua wakuu wa vikosi.

10 hWakati mtakapokwenda kushambulia mji, wapeni watu wake masharti ya amani. 11 iWakikubali na kuwafungulia malango yao, watu wake wote watawatumikia kwa kufanya kazi ngumu na watawatumikia. 12Ikiwa watakataa kufanya mapatano ya amani na wakiwaingiza katika vita, basi mtauzunguka mji huo kwa vita. 13 jWakati Bwana Mwenyezi Mungu wenu atakapouweka mji huo mkononi mwenu, waueni kwa upanga wanaume wote waliomo ndani yake. 14 kKwa upande wa wanawake, watoto, mifugo na kila kitu kingine chochote ndani ya huo mji, mnaweza kuvichukua kama nyara kwa ajili yenu. Nanyi mnaweza kuzitumia hizo nyara ambazo Bwana Mwenyezi Mungu wenu amewapa kutoka kwa adui zenu. 15 lHivi ndivyo mtakavyofanya kwa miji yote ambayo iko mbali nanyi, ambayo haimilikiwi na mataifa ya karibu.

16 mHata hivyo, katika miji ya mataifa ambayo Bwana Mwenyezi Mungu wenu anawapa kama urithi, msiache kitu chochote hai kinachopumua. 17Waangamizeni kabisa Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, kama Bwana Mwenyezi Mungu wenu alivyowaamuru. 18 nLa sivyo, watawafundisha kufuata mambo yote ya machukizo wanayofanya wakiabudu miungu yao, nanyi mtatenda dhambi dhidi ya Bwana Mwenyezi Mungu wenu.

19Wakati mtakapouzunguka mji kwa vita kwa muda mrefu, mkipigana dhidi yake ili kuuteka, msiharibu miti yake kwa kuikata kwa shoka, kwa sababu mtaweza kula matunda yake. Hivyo msiikate. Je, miti hiyo ya mashambani ni watu, hata muizingire? 20Hata hivyo, mnaweza kuikata miti ambayo sio miti ya matunda na kuitumia kujenga ngome, mpaka mji ulio katika vita na ninyi utakapoanguka.
Copyright information for SwhKC